HAKUJALI, HAKUTHAMINI, HAKUHITAJI, SASA WA NINI?

UNAPOMUWEKA mtu moyoni mara nyingi kumsahau ni vigumu. Wengi wanashindwa kuuona uzito huu kwa sababu hawakuwahi kupenda. Wanayachukulia mapenzi kama vile mchezo wa kuigiza. Yawepo sawa, yasipokuwepo pia sawa tu.
Thamani ya mapenzi anayeijua vizuri ni yule ambaye amekuweka moyoni. Huyo ndiye anaweza kuteseka kwa ajili yako. Yupo tayari kufanya lolote ilimradi tu kuhakikisha kwamba wewe mpenzi wake unakuwa na amani ya moyo.
Hayupo tayari kukuona unaingia kwenye msongo, kwenye raha mnakuwa pamoja na kwenye shida pia. Maisha ya uhusiano wa kimapenzi ndivyo yalivyo hivyo, kinyume chake huwa si uhusiano. Yanakuwa ni maumivu ya mapenzi.
Kila mmoja anafahamu maumivu ya mapenzi hasa kama utakuwa kweli umempenda mtu kutoka moyoni. Anapokuletea za kuleta, hakika maumivu yake huwa ni makubwa mno. Unatamani siku zirudi nyuma na muishi kwenye maisha yale mazuri mliyokuwa mnaishi.
Hapa ndipo kwenye hoja ya makala yangu ya leo. Najua kuna watu wameshawahi kukutana na kizingiti cha aina hii kwenye suala la uhusiano na wengine pengine sasa hivi ndiyo wapo kwenye mkwamo wa aina hii.
Unampenda mtu, unamhitaji, lakini inafika mahali hakupi ushirikiano mzuri. Hii ni mbaya zaidi kwa wale ambao tayari wanakuwa wameshaingia kwenye kifungo cha ndoa, hususan zile ndoa za Kikristo ambazo zina ugumu wa kufikia uamuzi wa kutengana.
Zile za Kiislam angalau, unapofikia kwenye hatua ambayo unaona hamuwezi kupikika tena chungu kimoja, basi mnaamua kuachana kwa heri na kila mmoja anashika njia yake, maisha yanaendelea. Kwa Wakristo mambo yanakuwa magumu kwani wao si rahisi sana kuachana.
Ndugu zangu, nataka nizungumze nanyi katika makundi yote mawili. Wale ambao ndiyo kwanza wapo kwenye hatua za uchumba na wale ambao tayari wameingia kwenye kifungo cha ndoa. Tukianza na wale wa kwenye uchumba au urafiki, wao kidogo kuna wepesi kwenye kufanya uamuzi sahihi.
Mpo kwenye hatua za mwanzo, mwenzako kwa maneno na matendo yake anakuonesha kabisa hakutaki, hakuthamini, hakuhitaji na hana mpango na wewe. Unapambana kwa kila hali ilimradi tu kuhakikisha unanusuru penzi lako, lakini mambo yanakuwa magumu.
Unajishusha, unahangaika kwa kila namna, lakini wapi. Mwenzako hana habari na wewe, hataki hata kukusikia. Hapo ndipo ninapokuuliza swali moja tu la msingi; “Sasa yeye ni nini?”
Kama mtu amefikia hatua hiyo fahamu kabisa ana sababu, hivyo hupaswi kuendelea kuumiza nafsi yako. Utaumia bure wakati mwenzako anaishi vizuri. Hatambui thamani ya penzi lako, achana naye. Kataa kuteseka, kataa kuishi kwa muda mrefu kwenye utumwa wa mapenzi. Utampata wako ambaye atatambua thamani ya penzi lako.
Kwa wale ambao mpo kwenye ndoa, hekima na busara zaidi inapaswa kuongezeka kwenu. Jitihada ya kunusuru penzi lenu zifanyike kwa gharama kubwa. Shirikisha wazazi, viongozi wa dini, wataalam wa saikolojia, watu waliokupita umri wenye uzoefu na mambo ya uhusiano na watu wengine unaoona wanaweza kutumia busara na hekima kurejesha uhusiano wako.
Ukiyafanya hayo yote na ikashindikana, muombe Mungu akusaidie kumfanya mwenzako ajue thamani ya ndoa yenu. Jipe muda mrefu bila kufanya uamuzi na ikishindikana hapo, fuata taratibu za imani yako kuibatilisha ndoa yenu na uishi kwa amani.
Tukutane wiki ijayo kwa mada nyingine nzuri.



No comments: