Wasichana mnaohamia kwa mabwana tuwaeleweje ?



Leo kwenye safu hii nimekuja na mada ambayo itawagusa wasichana wengi ambao uhamia kwa wanaume wanaowapenda na kuishi nao bila hata ya kujali kuwa dini hairuhusu.
Utakuta msichana anaanza kwenda kutembea kwa mpenzi wake wa kiume kwa kujifichaficha sana, anaanza kwa kutafuta visababu vidogovidogo mara anaacha rangi ya mdomo, siku inayofuata anaenda na pea mbili za viatu anaacha moja akijifanya amesahau.
Siku inayofuata tena ataamua kuongeza shuka kwani ataona shuka nyumbani kwa bwana hazitoshi, taratibu mwisho atahamishia kabati zima la nguo.
Hiyo haitoshi ataanza kwa kumnunulia vikombe mpenzi wake naye ataweka cha kwake mwisho wa siku kabati nalo litajaa vyombo kama vile tayari kaolewa anahudumia kwa mume.
Hii ni mbaya sana akina dada kwani inashangaza kuona mmeamua kujimilikisha wanaume kabla hamjaolewa, hivi hamuoni kila kukicha dharau ndiyo zinazidi mpaka ndoa siku hizi hazipewi kipaumbele kama zamani, unajua ni kwa nini? Kwa sababu wanaume wakitaka wanawake wanawapata kirahisi.

Nani wa kulaumiwa
kwa haya?
Kwa haya anayetakiwa kulaumiwa ni wazazi wa binti, baadhi ya wazazi wamekuwa wakikubaliana na hali ya watoto wao kuhamia kwa wanaume kwani akirudi nyumbani anampokea kama kawaida bila kumuuliza alikuwa wapi.
Wengine wanapokea hata hela wanazoletewa na binti kutoka kwa mwanaume husika na mtoto akitaka kwenda kulala anamuaga mama na kumuacha amekaa sebuleni bila kujiuliza ni kwa nini mwanangu ameamua maisha haya au hata kuwa mkali basi maana mtoto umleavyo ndivyo akuavyo.

Kinachouma sasa
Kinachouma kwa mabinti zetu hata ukiamua kuhamia kwa mume unakuwa huna cha kushika wala huna haki yoyote akiamua kukufukuza muda wowote anakufukuza kwani hana ndoa na wewe.

Je, utamshtaki wapi?
Kumbuka kuwa huna pa kumshtaki kwani hata ikitokea mmegombana ugomvi wenu pa kukimbilia huna kwa sababu uhusiano wenu siyo rasmi.
Ikitokea maafa mko
wote ndani?
Hivi ujiulize ikitokea maafa uko ndani na mpenzi wako halafu amefariki dunia na wazazi wake hawakujui utafanya nini? Huoni kama utakosa pa kuanzia na huenda kesi ikawa ya kwako.
Kwa leo nimeona niwakumbushe hili kwani naona ni kama fasheni wasichana kuhamia kwa wapenzi wao.




No comments: