MREMBO WA WA KIJIJI SEHEMU YA KUMI NA TATU-13




MREMBO WA WA KIJIJI

 SEHEMU YA KUMI NA TATU-13

"Nani huyo kacheka?.." Aliuliza Saidon baada kusikia kicheko nje. Maige akaguna kisha akajibu kwa sauti ya chini "Chaudele huyo, yani tumemtaja tu naye katokea. Sasa sijui kafuata nini"

"Wee unasema kweli?.." Saidon alipigwa na mshangao, punde si punde akanyanyuka akatoka ndani. Alipofika mlangoni ghafla akashtuliwa, aliyemshtua hakuwa mtu mwingine bali ni Chaudele. Ambapo binti huyo mara baada kumuona Saidon kashtuka aliangua kicheko, kicheko ambacho kilimfanya Saidon kutabasamu huku moyoni akijiuliza "Inamaana ule msemo kwamba mbuzi kafia kwa muuza supu ndio umetimia?.." Kabla hajapata jibu la swali hilo alilojiuliza, Chaudele alimsabahi  "Mambo"

"Poa mzima" Alijibu Saidon.

"Mimi mzima, mbona umeadimika sana?.." Alirudia kuuliza mrembo Chaudele, safari hiyo aking'ata kucha huku uso wake ukitawaliwa na haya, kimtazamo binti huyo akionyesha kubeba kusudio fulani ila aliogopa kulitoa kwa kijana bishoo kutoka jiji la Bandari.  Saidon alishusha pumzi kidogo halafu akajibu "Aha jana tu? Lakini mimi nipo siku zote na nitaendelea kuwepo hapa Ndaulaike"

"Sawa asante, nilipita kukusabuhi tu" Aliongeza kusema Chaudele kisha akaanza kuondoka zake. Saidon aliishia kumtazama tu wakati huo akionekana kutaka kusema jambo hali ya kuwa moyo wake ukisita kutoa maamuzi sahihi. Hivyo aliishia kumtazama tu, lakini mwishowe uvumilivu ulimshinda ambapo akaamuwa kuvunja ukimya na kisha kusema "Unaonaje nikusindikize?.."

"Ahahaha hahaha" Aliangua kicheko Chaudele kisha akajibu "Hapana utanisindikiza siku nyingine" Maneno hayo yakahitimishwa na tabasamu bashasha kutoka usoni mwa mrembo huyo wa kijiji, mrembo mtamu vilivyo kwa jinsi alivyo umbika.

Saidon alikubaliana na matakwa ya Chaudele, alimpungia mkono wa kwaheri kisha akarudia ndani. Alipofika alikuta tayari Maige kamaliza kusonga ugali na hivyo sufulia yenye mboga liliwekwa jikoni ili kupasha. Saidon aliketi kwenye kigoda, akiwa na tabasamu pana mithili ya changudoa aliye ona kitita cha dola. Alishusha pumzi kidogo kisha akasema "Unajua ndugu yangu Maige waswahili wanasema, kibaya cha jitembeza ila chema chajiuza"

Maige alicheka kidogo halafu akauliza"Unamaana gani Saidon?.."

"Maana yangu ni kwamba Mimi ni kama kitu chema, kwahiyo najiuza ila yule ambaye ukoo wao wote wanga, ni kitu kibaya kwahiyo chajitembeza" Alijibu Saidon.  Jibu hilo lilimshangaza kwa mara nyingine Maige, hapo akaonakana kama kutomuelewa vilivyo Saidon. Hivyo kwa taharuki kubwa akarudia kumuuliza "kwahiyo ndugu yangu unataka kusindana na Chitemo?.."

"Amini hivyo Maige, mimi nimeshakwambia kuwa siku zote uchawi hauji kwa mentali"

"Sawa ndugu yangu hapo mimi sitii neno, enhe kwahiyo Chaudele kafuata nini?.."

"Chaudele hajafuata kitu ila alikuja kunisabahi mara moja, hapo ndio utajua kwamba mimi nitafanikiwa kumtwaa Chaudele bila ndumba bila pesa. Ahahah haha tule chakula bwana Maige ila mwaka huu atapata tabu sana" Alihitimisha Saidoni. Wakati huo huo upande wa pili nyumbani kwa mzee J, hali ilioneakana kuwa shwari kwa kijana wake wakuitwa Chitemo. Chitemo alikuwa amepoteza fahamu kwa takribani masaa kadhaa baada kukumbana na balaa la bibi Pili. Jambo hilo la kuzinduka Chitemo lilimfurahisha sana mzee J, hapo akamtaka mkewe apike uji haraka sana uwezekanavyo. Kitendo hicho kilitekelezwa, Chitemo akanywa uji kisha akalala ili kuyatuliza maumivu aliyokuwa akiyasikia sehemu mbali mbali ya mwili wake.

 Kipindi kijana Chitemo alipokuwa amelala huku akisafa na maumivu yake, mzee J nae aliendelea kujipa tiba. Wakati mzee huyo anajitibu, akamgeukia mkewe na kisha akasema "Unajua mke wangu, nzi akiacha ujinga anaweza kutengeneza asali"

Mama Chitemo alipoyasikia maneno hayo akasitisha zoezi la kupuliza moto akamgeukia mumewe na kumjibu "Ni kweli kabisa baba Chitemo, ila sijajua unamaana gani kusema maneno hayo"

 Mzee akacheka kidogo halafu akasema "Huwezi kunielewa mke wangu, ila huu ni wakati wa kumjibu mzee Nhomo juu ya posa yetu. Na ukiachana na hayo bwana mke wangu, namngoja Chitemo awe Sawa ili aniambie ni nani aliyefanya kitendo hiki. Nikimjua tu ama zake ama zangu"

"Kweli kabisa baba Chitemo, huu siuungwana kiukweli" Aliunga mkono mama Chitemo kisha akaendelea kuchochea kuni huku juu ya mafiga pakiwa na jungu kuu lililojaa viazi na karanga. Hapo maongezi mawili matatu yakafuatia baina ya mzee J na mkewe, lakini  ghafla maongezi yao yalisitishwa na sauti nene iliyokuwa ikisikika. Sauti ambayo ilifanana na mlio wa wa kundi la nyuki, punde si punde juu angani lilioneka tunguli kubwa mfano wa mtungi.

 Tunguli hilo lilikuwa limezungushiwa shanga za rangi tofauti tofauti huku kwenye mdomo ukifuka moshi. Mzee J alipoliona tunguli hilo alimuhimiza mkewe akimbie ndani haraka amletee jungu lake analohifadhia mazaga ya kichawi. Mama Chitemo alifanya hivyo, hima alitoka nalo ndani na kisha kumkabidhi mumewe. Mzee J akalipokea kwa utashi na kujiamini, akakava hirizi na kujipaka dawa sehemu mbali mbali za mwili wake, alipokamilisha zoezi hilo kicheko kikasikika kutoka ndani ya lile tunguli lililoonekana angani.

"Ahahaha hahaha hahaaaa"

 "Jaruooo unavita kubwa sanaaaa, na vita hii kamwe hutoweza kushinda kwa sababu unapambana na majeshi mawili tofauti. Na yote yananguvu" Sauti nzito iliyo kuwa ikijirudia mara mbili mbili ilisikika ikisema punde tu ilipo hitimisha kicheko.

Mzee J alipoyasikia hayo maneno,  kijasho kikaanza kumtoka wakati huo akijiuliza nani tena kaongezeka kwenye  vita hiyo baina yake na mzee Nhomo? Kabla hajapata jibu la swali hilo alilojiuliza mara ghafla tunguli lile likaangua kicheko kwa mara nyingine. J akashtuka huku akitetemeka mwili mzima, akiwa amejawa na hofu dhofu lihali akauliza" Kwahiyo nifanyeje mimi naombeni msaada wenu "

" Hahahahah hahahah! Jaruooo msaada upo, ila utatakiwa kutoa damu" Liliongea tunguli.

"Ndio ni.. Nipo.. Nipo tayari kwa lolote mladi nitimize matakwa yangu" Alikubali mzee J, punde si punde kibuyu kidogo kilidondoka kutoka kwenye tunguli lile. J mahali akanyanyuka akakifuata kibuyu hicho, alipokitwaa mikononi mwake tunguli lile likaongeza kusema "Mimina humo damu utakayo ipata, kibuyu hicho tembea nacho pindi unapokuwa uwanja wa vita. Kunywa tonya moja kila baada ya dakika tano, hakikisha haikauki ndani ya kibuyu hicho..."

" Sawa Sawa wakuu"  Aliitikia mzee J, tunguli nalo likapotea angani. Hapo mzee J akashusha pumzi ndefu huku kijasho kikimtoka akavua hirizi zake kisha akazirudisha ndani ya chungu chake. Baada ya hapo akamuita mkewe, mama Chitemo  akatii wito.

" Mke wangu, nilicho kuwa nakisema ndicho kilichotokea "

" Unamaana gani baba Chitemo?.. " Alihoji mama Chitemo huku akiwa amejawa na taharuki. Mzee J akashusha pumzi ndefu kwa mara nyingine kisha akajibu  "Sipambani na Nhomo tu, kuna mjinga mwingine kajitokeza. Sijui ni nani? Ila ngoja Chitemo akiamka ataniambia kila kitu. Sitaki kuchezewa mimi" Alighadhibika mzee J.

Wakati mzee J akifahamu ukweli uliokuwa ukisumbua akili yake juu ya mapigano yanayo endelea, kwingeneko pindi mzee  Mligo yupo njiani akikikaribia kijiji cha pili alichokwenda kwa niaba ya masuala ya soka,  ghafla mbele yake akatokea mzee Bidobido mdogo wake mzee J. Mligo akajikuta akiweweseka na baiskeli yake kiasi kwamba alikosa umahili wa kujizuia akawa ameangukia polini. Aliponyanyuka akafoka, akasema "We vipi umawazimu? Ningekugonga? Jeheshimu bwana" Maneno hayo aliyasema huku  akiinyanyua baiskeli yake ili aendelee na safari. Lakini kabla hajajiandaa ili apande, mzee Bidobido akamnyooshea kidole kisha akamwambia "We mzee wewe, mwambie mjukuu wako afanye alichokifuata hapa kijijini. Aachane kabisa na Chaudele, la sivyo ataangukia pabaya" Kwisha kusema hayo akapotea ikabakia vumbi. Jambo hilo lilimshangaza sana mzee Mligo,  alijiinamia na kujiuliza maswali kuhusu mzee huyo aliye mtokea na kupotea kimazingira mbele ya mboni zake, lakini pia alijiuliza mkwala huo kuhusu Chaudele binti Nhomo. Alikosa majibu zaidi akajisemea  "Mmh hili nalo balaa sasa. Ila asinitishe kitoto mimi, kama noma na iwe noma tu"

"Asinichukulie mimi nanga" Aliongeza kusema mzee Mligo, punde tu Bidobido akatokea kwa mara nyingine tena huku akipiga makofi na kuachia tabasamu la kinafiki.  Lakini mzee Mligo hakutishika na ujio wa mara ya pili huo, zaidi akataka kumthibitishia kuwa hata  yeye sio mtu wa kubeza. Hivyo alipiga mguu wake wa kushoto chini mara mbili kisha akapotea na baiskeli yake, ikasilia vumbi tu na milio ya bundi. Bidobido akaraharuki, akatangaza macho yake kutazama huku na kule wakati huo asiamini kama kweli mzee Mligo naye si wa mchezo. Muda mfupi baadaye naye akatoweka mahali hapo. Baada ya dakika kadhaa mzee Mligo akatokea akacheka sana kwa dharau kisha akasema "Mlijua mimi kiazi! Haya nzeni wenyewe sasa"

    DADEKI HUU MOTO USISIMULIWE SOMA MWENYEWE 😋
  KIPI KILIJILI HAPO HAPO? habari wanayo..
SHEA MARA NYINGI ILI NIKUTUMIE MUENDELEZO INBOX, mlio Shea nazani mliona sasa sijui nyie wengine mnakwama wapi kukosa kigongo hiki.. MLIJUA KIAZI? 😂



No comments: