MREMBO WA WA KIJIJI SEHEMU YA YA KUMI NA TANO-15



MREMBO WA WA KIJIJI


      SEHEMU YA YA KUMI NA TANO-15

Bibi Pili aliposikia wenzake wametua nje ya nyumba yake, alitoka ndani upesi. Alikuta umati wa wachawi ukiwa umeketi chini na nyungo zao wakimngoja kwa hamu,  alitabasamu kidogo kwani alijua kuwa tayari muda umefika wa kufanya kazi maalumu iliyokuwa ikiwakabili mbele yao. Hivyo kabla hajafanya jambo lolote, alirudi ndani moja kwa moja akamsogelea Pili kisha akamgeuza namna ya kulala. Alipokuwa amelala kichwa ikilazwa miguu, na ilipokuwa imelala miguu kikalazwa kichwa. Baada ya hapo alicheza huku akiimba nyimbo zake za asiri. Alipomaliza kuimba akapotea  ndani akaibukia nje ambapo aliweza kuungana na wachawi wenzake. Alifanya vile kumzindika Pili ili asishtuke kutoka usingizini mpaka pale atakapo rejea.

  "Bibi Pili, tumekuja kwa mara nyingine tena. Safari hii tunaenda kuchukuwa mkewe J ili tumuadabishe kisha mwisho tunamalizia na mzee J mwenyewe, tumezamilia sana kufanya mambo haya sifikirii kama kati yetu kuna mtu anaogopa kupambana. Lakini pia baada kufanya haya, hatutoishia hapo bali tutaanza kuua mmoja baada ya mwingine ama mnasemaje?.. " Alisema kiongozi wa kundi hilo la wachawi. Hakuna mchawi aliyejitokeza kuhofia vita hiyo. Hivyo kiongozi huyo baada kuona hakuna mtu aliyetia shaka, alikohoa kidogo kisha akaongeza kusema " Vizuri sana, sasa hapo mnanipa matumaini. Kwahiyo hakuna muda wa kupoteza. Kila mmoja ajiandae kikamlifu. Tunadakika tano tu za kujizatiti"

Alipokwisha kusema hayo kiongozi wa msafara, haraka sana wachawi wote waliokuwepo mahali hapo wakaanza kujifunga vizuri hirizi zao huku wengine wakionekana kunywa damu zilizokuwemo kwenye vibuyu vyao. Muda ule aliotoa kiongozi wao ulipokwisha akaanza kuhesabu namba moja mpaka tano, akiwa na maana kuwa pindi atakapo fika tano tu mara moja waanze safari kuruka angani kwa kutumia ungo. "Mojaaa...mbili..tatu...nne..tanoooo" Wachawi hao kundi lakina bibi Pili lilianza safari, waliruka kwa pamoja mfano wa ndege waliotimuliwa kwenye shamba la mpunga. Mbwembwe za hapa na pale walizionyesha walipokuwa angani, vijana wenye nguvu waliziyumbisha nyungo zao kwa kuzilaza kulia na kushoto kuzipandisha juu na chini mfano wa mbayu wayu warukavyo, zote hizo zikiwa ni rasha rasha za kufurahia safari ya kuvamia nyumbani kwa mzee J. 

Huku nyumbani kwa mzee Mligo, baada kuona shehena la wachawi wanakuja nyumbani kwake alizama uvunguni mwa kitanda chake akatoka na mkoba ulionekana kuchakaa, sababu tayari bui bui walikuwa wameshajijengea makazi. Mkoba huo ulichakazwa na utandu ilihali buibui watoto nao wakitoka kwenye mifuko ya pembeni. Mligo alipoushika vizuri akaukung'uta vumbi kisha akasema "Wamefufua makaburi ya zamani, sasa acha niwape wanacho kitaka"

Alipokwisha kusema hayo akaingiza mkono kwenye mkoba wake akatoka na hirizi kubwa akajifunga mkono wa kushoto "Naam siku zote moto hautishwu na makalio ya sufulia " Aliongeza kusema mzee Mligo, safari hiyo alimgeuza mjukuu wake wakuitwa Saidon. Kichwa akakilaza inapo lala miguu, na miguu ikalazwa mahala inapo lala kichwa halafu akamwagia dawa ambayo ilimfanya Saidon kulala usingizi mzito uliojaa ndoto za ulimwengu mwingine kabisa.

 Hata kilichokuwa kikitokea hakuweza kukiona. Punde baada kufanya hayo, nje ya nyumba yake timu ya mzee J ikatua. Siku hiyo walifanikiwa kuikuta nyumba ya Mligo, hivyo jambo hilo likawa jambo la heri kwani waliamini kuwa safari hiyo wataweza kutimiza azma yao.

"Kila mmoja yupo tayari?.." Aliuliza mzee J.

"ndio mkuu"  Walitikia wachawi hao.

 "Sasa naomba tuyaandae makombora yetu, kwa vyovyote kwa lolote lazima kila kitu kiende sawa" Amri hiyo iliyotoka kinywani kwa mzee J iliwafanya hao wachawi kutoka kwenye nyungo zao kisha wakazipoteza kimazingara wakasalia wao kama wao huku wakionyesha utayari wa kukabiliana na mzee Mligo ingawa dhumuni lao kuu ikiwa ni kutaka damu ya Saidon vile kumjaribu kutokana na ugeni wake.

    ********
Upande wa pili, lilionekana kundi la kina bibi Pili likiambaa kuelekea kwa mzee J. Lakini kundi hilo lilipokuwa angani, mara ghafla mzee Nhomo alionekana nyuma yao akiwafuata. Mchawi mmoja aliyekuwa nyuma machahale yakamcheza akahisi nyuma yake kuna mtu anawafuatilia, punde si punde akageuka nyuma akamuona Nhomo.

"Huyu anataka nini? Ngoja nimuadabishe kwanza asije leta balaa hapa"  Alisema   mwanakikundi mwenzake bibi Pili. Papo hapo akaguza akarudia kule anakotoka akimfuata mzee Nhomo, muda huo huo akamrushia makombora. Nhomo alijitahidi kuyakwepa, alipoona mambo yanenda kuwa magumu haraka sana naye akajibu mashumbulizi. Hapo sasa ikawa piga nikupigie kila mmoja alionyesha umwamba wake, lakini mwisho wa yote Nhomo alifanikiwa kumtungua adui yake. Kitendo ambacho kilichopelekea yule mchawi kuanguka chini,  aliachia tabasamu mzee Nhomo baada kufanikisha jambo hilo, ndani ya nafsi yake akajisemea "Sio kila siku ni juma pili, sasa leo nitakula nanyi sahani moja kudadeki. Nitawadondosha mmoja baada ya mwingine"

"Upele umepata mkunaji" Aliongeza kusema mzee Nhomo wakati huo akiukimbiza ungo wake kwa kasi ya ajabu akiwafuatilia wale wengine.
  "Mkuu tumefika salama lakini kuna mmoja wetu haonekani"  Ilisikika sauti ya binti mmoja ambaye naye ni moja ya wachawi. Binti huyo alikuwa akimuasa mkuu wake mara baada kufika nyumbani kwa mzee J. Mkuu huyo alishtuka, akawatazama watu wake wote kisha akasema "Moja.. Mbili Tatu.. Nnee, nyie nendeni mkamfuate mwenzenu. Wawili piteni anga ya juu, pia wawili piteni chini"

"Sawa Sawa mkuuu" Walitikia wachawi hao walioteuliwa kumfuata ndugu yao aliyetunguliwa na mzee Nhomo pasipo wao kujua. Wakati huo kabla mzee Nhomo hajatua kwenye himaya ya mzee J, ghafla alisikia sauti nene ikisema "Nhomo, huwezi kukabiliana na umati uliopo hapo. Unaitaji nguvu ya kutosha" Mzee Nhomo aliposikia sauti hiyo alishtuka, akiwa na hofu akauliza "Kwanini sasa? Wakati nilishakuja kwenu kwa dhamira ya mimi kushindana na huyu mwanaharamu?"

"Aha hahahah" Suti hiyo iliangaua kicheko halafu ikaongeza kusema "Usilo lijua ni usiku wa giza.."

"Unamaana gani?.." Nhomo Alirudia kuhoji.

Sauti hiyo ikamjibu kwa mkato kisha ikapotea "Rudi nyumbani kesho njoo kilingeni ili tukupe uwezo mara mbili ya ulio nao ili mambo yako yaende sawa"

"Doh sawa" Alisema mzee Nhomo kisha akageuza muelekeo, akaanza kuelekea nyumbani kwake, lakini kabla hajafika mara ghafla nyuma yake ilioneakana miale miwili ya moto ikimfuata nyuma. Nhomo alipoiona akajua dhahili shahili maadui wanamfuata, hivyo aliongeza kasi ya kuwakwepa ingawa bado kasi yake ilioneakana hafifu, miale hiyo ya moto ilizidi kumkaribia zaidi.

 "Ukisikia kufa kiume ndio leo sasa, na hawa jamaa sijui wakijiji gani" Alijisemea mzee Nhomo akishangazwa na uwezo wa wachawi hao. Na wakati huo Nhomo anafatiliwa, huku nyumbani kwa mzee J tayari mama Chitemo alikuwa ameshatolewa ndani. Aliwekwa kati, nyimbo ndelemo zikatawala, punde si punde mkuu wao akatuliza ndelemo hizo kisha akasema "Wananzengo tayari mama wa yule kijana mshenzi mchezea mabinti tunaye hapa, sasa basi nyie pandeni usafiri wanu wa kawaida ila mimi nitamgeuza huyu mtu kuwa ng'ombe, mpaka nyumba kwa bibi Pili kisha mengine yaendelea" Alisema mkuu wa msafara, lakini kabla hajafanya muujiza huo ghafla...






No comments: