MREMBO WA WA KIJIJI SEHEMU YA YA TISA-09




MREMBO WA WA KIJIJI

      SEHEMU YA YA TISA-09

Walisikia mvumo mkali wa Upepo ukiwafuata, na punde si punde bundi mkubwa aliwapita kwa kasi ya ajabu. Mzee J alishtuka, hapo akachukua kibuyu chake akakitikisa. Kibugu hicho kikalia "Kuchu kuchu kuchuuuuu" Aliposikia mlio huo, aliachia tabasamu kisha akafungua mdomo akajimiminia damu, nyingine alichovya kipisi cha mkia wa ng'ombe halafu akanyunyuzia kila pande kuu nne za dunia. Kitendo hicho kilileta amani, dhoruba ile iliyo kuwa imetokea muda mchache uliopita ilitoweka.

"Mkuuu wewe ni noma " Alisema kijana mmoja aliyeonekana ndani ya ungo, kijana huyo alikuwa akimsifu mzee J kwa kuwezaa kuzuia balaa lilolotaka kuwa haribia safari yao. Mzee J aliposikia sauti hiyo aligeuka upande wake wa kushoto akamuona kijana ambaye ni mwanachama wake, hapo alicheka kidogo kisha akamuonyeshea kidole gumba. Baada ya hayo aliulaza ungo wake kwa kuukata Upepo, hali hiyo ikaifanya nyungo za hao wachawi kulipendezesha anga kana kwamba ni ndege wale wasafirio umbali mrefu kwa makundi. Lakini kabla mzee J na kundi lake hawajafika nyumbani kwa mzee Mligo kwa nia ya kumfuata kumjaribu mjukuu wake, yule bundi aliwapita kwa kasi ya ajabu alitua kwenye paa la nyumba ya mzee Mligo. Akatoa mlio fulani ulioweza kumuamsha mzee Mligo usingizini, haraka sana mzee huyo akatoka ndani. Alipofika nje, alitazama juu ya paa ya nyumba yake, punde si punde yule bundi akatua kwenye bega lake. Upesi alimkamata kisha akamtazama kwenye macho yake yaliyoonekana kung'aa kama macho ya paka pindi atazamapo mwanga.

 Mara ghafla Mligo akajikuta akitaharuki, alichokiona kwenye mboni ya bundi kilimshtua, hivyo hakutaka kupoteza muda alimuachia bundi wake kisha akaingia ndani akachukuwa hirizi kubwa iliyokuwa uvunguni mwa kitanda chake. Alipoipata alitoka ndani wakati huo akiwa ameshika kisu. Akiwa na hofu dhofu lihali,  Mligo aliipasua hirizi hiyo katikati. Ndani ya hirizi hiyo palikuwa na mifupa ya mijusi vile vile ulikuwemo na unga mweusi.  Aliitoa mifupa hiyo akaitupa juu ya paa kisha akausogelea mlango wa nyumba yake akaingia ndani kinyume nyume, akachukuwa na ule unga mweusi akautupa nje kitendo ambacho kilipelekea nyumba kutoweka kimazingira likaonekana bwawa huku sauti za vyura zisikika kila pande.

Na wakati nyumba ya mzee Mligo inatoweka, kundi la wachawi likiongozwa na mzee J lilitua kwa wingi mfano wa ndege watuavyo kwenye shamba la mpunga.

"Mkuuu mbona nyumba hatuioni" Aliulaza mchawi mmoja.

 Mzee J hakujibu maana muda huo alionekana kama kapagawa. Wakati huo huo mchawi wa pili ambaye alionekana bibi kizee, naye alisema "Ama tumetua sehemu ambayo sio sahihi? Maana sioni nyumba naona bwawa tu hapa"

"Shiii kaeni kimya, sio mnaongea ongea tu ebo" Aling'aka mzee J, aliwaasa wananzengo wake wakae kimya muda huo akifanya mambo kimya kimya kwa dhumuni la kuitafuta nyumba ya mzee Mligo. Na kipindi hayo yote yanatokea, upande wa kijana Saidon alikuwa hajui chochote kinachoendelea. Bali yeye alikuwa amelala usingizi mzito huku ndoto mfululizo zikifuatana kichwani mwake, ndoto zote zilikuwa za kutisha kwani ndivyo inavyokuwa pindi unapoingiliwa na wachawi iwe ndani ama popote pale hasa ukilala usingizi, ndoto za kutisha ndizo zitakazo kueleza kuwa mahali ulipo kuna mchawi. Saidon moja ya ndoto aliyoota ni kudondokea kwenye shimo lisilokuwa na mwisho, na sio hiyo tu aliota pia yupo msituni anakimbizwa na kiumbe cha ajabu, lakini yote hayo ni kwa sababu jopo la wachawi tayari walikuwa wamevamia nyumbani kwa babu yake istoshe pia babu yake naye tayari alikuwa ameshaiweka nyumba yake katika hali ya kichawi.    Baada ya muda wa nusu saa J alipasa sauti akasema "Aloh ama kweli umzaniaye ndio kumbe sio, na umzaniaye sio kumbe ndio. Nimemkosa mzee Mligo, na hiyo ni kutokana kutomfahamu vizuri mzee huyu sababu laiti kama ningejua kuwa naye yumo kwenye haya masuala basi ningejiandaa vizuri"

"Kwa hiyo mkuuu tunafanyaje?.." Aliuliza Mwananzengo mmoja baada kuyasikia maneno ya mkuu wake.

 "Hakuna cha kutupotezea muda, tuondeke mahali hapa. Lakini tusiondoke hivi hivi. Masumbuko achia mdondiko tucheze kwanza" Alijibu mzee J wakati huo akimtaka mzee Masumbuko apige ngoma ili wapate kucheza.

 "Ahahahahah hahahah" Alicheka Masumbuko kisha akanyoosha kidole mbele yake, ghafla ikatokea ngoma. Shangwe zililipuka maeneo hayo, na punde si punde mdondiko ulisikika wachawi hao wakaanza kuimba na kucheza.

  Upande wa pili nako mzee Nhomo alionekana akijiandaa  kichawi kwa niaba ya kumfuata mzee J nyumbani kwake ili athibitishie kuwa haogopi mkwala anaotangaza kijijini. Kwa maana hiyo yupo tayari kwa chochote kile.

 "Nataka nimuonyeshe utofauti wa mimba na ujauzito, asinione mnyonge mimi. Yani mtu mzima tangu lini akatishiwa nyau?.." Alijisemea mzee Nhomo wakati huo akijifunga madhubiti hirizi yake ikiwa moja ya maandalizi ya kuelekea nyumbani kwa mzee J. Alipokwisha kusema hayo na kukamilisha vizuri maandalizi hayo, akanyoosha kidole mbele yake ambapo ulitokea ungo mkubwa kiasi ulioonekana kuwa na mapana ya kutosha. Ungo huo ulikuwa wa rangi nyeusi,  Nhomo alitabasamu baada kuuona ungo wake kisha akacheka halafu akazipiga hatua kuusogelea. Alipoufikia alitazama Kwanza kulia na kushoto, alipoona hali ni shwari akapanda na kisha kunuia maneno ya kwenye ngome yao ya kichawi. Mwisho wa yote ukatokea upepo mkali ukaunyanyua ungo huo na safari ikawa imeanza kuelekea nyumbani kwa mzee J.

Lakini pia wakati mzee Nhomo yupo angani, kwingineko kundi la wachawi lilitua nyumbani kwa bibi Pili kwa dhumuni la kuunganaa pamoja kumfuata mzee Chitemo ili wakampe kipigo cha mbwa koko. "Jamani kama tulivyokubaliana, Sasa huu ndio muda wa kuelekea kwa mzee J ili tumuadabishe kijana wake. Mpango huu ni kama kumuunga mkono mwanachama mwenzetu hapa bibi Pili hivyo kila mmoja ajiandae kwa safari ikiwezekana hili zoezi tulimalize kabla hata hapajapambazuka" Alisema kiongozi wa msafara uliotua nyumbani kwa bibi Pilil.

 "Sawa sawa mkuuu" Waliitikia wachawi hao, na muda mchache baadaye wakaonekana angani wakielekea kwa mzee J.  Anga la kijiji cha NDAULAIKE sasa likawa limegubikwa na nyomi ya wachawi kwani wakati kundi hilo la kina bibi Pili na mzee Nhomo walipokuwa angani wakielekea nyumbani kwa mzee J kwa nyakati tofauti, upande wa pili nako, mzee J naye alikuwa  angani na jopo lake kwa kasi ya ajabu hasa baada kuwaasa wananzengo wake kwamba anahisi kuna hatari inakaribia kutokea nyumbani kwake. Kwa hiyo kasi hiyo ya ajabu ilikuwa ni kwa niaba ya kuiwahi hatari hiyo kabla mambo hayajaharibika.

  HAWA JAMAA WANAKUTANA SEHEMU MOJA.. Kipi kitaendelea? Hayo na mengine mengi tukutane sehemu ijayo.
   Usisahau kushea ili usipitwe na sehemu nyingine.



No comments: