MPENZI CHEUPE 04





Alikutana na vifaranga vya kuku kama kumi,vilikuwa vidogo vyenye umri kama wa siku moja au mbili tangu kutotolewa,Brown alishtuka sana,macho yalimtoka,mapigo ya moyo yalizidi kwenda mbio,alijuwa ni ni mtu amegonga alipochelewa kufungua ndipo aliweka wale vifaranga,aliinama ili akishike kimoja,ghafla vilipotea,Brown alirudi mbio ndani kwake na kujifungia,akiwa bado amesimama hajui la kufanya,alisikia vyombo vikianguka jikoni,aliogopa kwenda,aliamua kuingia chumbani kwake na kujifungia,alijifunika shuka gubigubi na kupitiwa usingizi.

Asubuhi alipoamka alikwenda kuchemsha chai ili apate kifungua kinywa,wakati chai inachemka aliwaza "hiki kinachotokea kwenye maisha yangu ni nini? au kweli Salma ni mzimu?" yalikuwa maswali bila majibu kichwani mwa Brown,chai ilichemka alimimina na kuketi mezani akanywa chai,alipokaribia kumaliza aliona pembeni ya meza karatasi nyeupe imekunjwa vizuri,aliichukuwa na kuikunjua aliona imeandikwa "mpenzi mpishi mzuri wa chai,asante kwa kifungua kinywa,siku nyingine ongeza na viungo ili inoge zaidi,wako mpenzi Cheupe" jasho jembamba lilikuwa likimtoka Brown "ina maana nipo kwenye hatari,nimtafute yule dereva tax huenda akawa na majibu sahihi" Brown aliongea mwenyewe kama kichaa.

Alijiandaa na kutoka kuelekea mtaa wa Aggrey,alipofika alikuta tax nyingi sana,aliulizia kwa kutaja muonekano wa yule dereva tax,ilikuwa vigumu kumpata "mbona hakuna mtu kama huyo hapa" Brown alijibiwa na mmoja wa maderava tax,alikata tamaa ya kumuona,wakati anaondoka alipofika karibu na Mnazi Mmoja aliomuona yule dereva tax alikuwa na abiria wenye asili ya Asia,alipotaka kusogelea ile tax ilianza kuondoka,alijaribu kuifuata bila mafanikio,aliamua kurudi nyumbani kupumzika akiwa mwenye lindi la mawazo.

Brown alipokaribia nyumbani alipatwa na mshtuko mkubwa baada ya kuiona ile tax imepaki mbele ya nyumba yake,alipiga hatua za haraka kuiendea ile tax,alipokaribia ile tax ilianza kuondoka "mh ! hii sasa maana yake nini? nipo macho naota?" alijiuliza maswali katika hali ya kutoamini anachokiona,maisha yake sasa yalijawa na mauzauza,aliamua kutulia nyumbani,mpaka giza lilipoingia,alienda kwa mama ntilie kula na kurudi kulala,siku ilikuwa mbaya kwake,alilala katika hali ya unyonge sana mpaka palipo pambazuka hapakuwa na kituko chochote,alijiandaa kwenda kwenye biashara zake,alifika kituoni kusubiri Basi kama abiria wengine,Basi lilifika,lilikuwa tupu,abria wote walikuwa pale kituoni  walipanda.

Basi liliondoka kuelekea katikati ya jiji,cha ajabu lilipita vituo vyote bila kusimama,Brown alishangazwa na mwenendo wa lile Basi ndipo aligundua kuwa halikuwa na kondakta,wakati akiendelea kujiuliza mara abiria wote waligeuka kumwangalia,hawa kumsemesha neno lolote,Brown alipigwa butwaa alipo ona sura za kutisha za watu aliokuwa akiwafahamu ambao walishakufa miaka mingi iliyopita,mapigo ya moyo yalimwenda mbio nusu yasimame kwa woga,alikuwa ameketi kwenye siti ya nyuma kabisa "hiki nini tena!" alitamani kushuka lakini alijiuliza atawapitaje wale watu,haja ndogo ilimtoka bila kujijua,utanashati wote ulimwisha,mara lle basi lilisimama katikati ya msitu,wale watu walimgeukia tena kumwangalia,alielewa kuwa walimtaka ashuke,Brown alishuka,mmoja wa wale watu alimsukuma singi kama vile alimwambia usirudie tena.

Palikuwa ni mazingira ya kutisha sana,msitu mnene kiasi gari ziliwasha taa machana kupita eneo hilo,Brown akiwa katika hali ya woga na kutetemeka Basi liliondoka na kumwacha peke yake pale msituni,ghafla alisikia upepo mkali ukivuma,hali ya giza iliongezeka,radi zilipiga kwa fujo,Brown akiwa amesimama hajui wapi pa kuelekea,ghafla alimuona mtu amesimama mbali kidogo na pale alipokuwa Brown,alikuwa amevaa nguo nyeupe sana,alimpa Brown ishara amfuate kuelekea kule lilipotoka Basi,Brown alijuwa anaonyeshwa njia ya kutoka pale msituni na kumbe.............ITAENDELEA



No comments: